Jumapili, 27 Novemba 2016

UBOVU WA MIUNDO MBINU HIFADHI YA TAIFA YA RUAHA WAIKOSESHA MAPATO SERIKALI

Baadhi ya waandishi wa habari wanawake kutoka katika vyombo mbali mbali na mikoa tofauti nchini Tanzania wakiwa katika picha ya pamoja na Kaimu Muhifadhi Mkuu wa Hifadhi ya Taifa Ruaha bw. Moranda B. Moranda, hivi karibuni baada ya kutembelea hifadhi hiyo.
Kulia  ni Kaimu Mkuu Muhifadhi wa Hifadhi ya Taifa Ruaha bw. Moranda B. Moranda, kushoto ni bi. Esther Macha mwandishi wa gazeti la Majira na  mwenyekiti wa Umoja wa Waandishi wa Habari Wanawake nchini,    



Imeelezwa kuwa changamoto kubwa inayokwamisha shughuli za kitalii katika Hifadhi ya taifa ya Ruaha na kupelekea serikali kukosa mapato  ni  ubovu wa miundo mbinu.

Hayo yameelezwa na Kaimu Mkuu wa Hifadhi ya Ruaha bw. Moranda B. Moranda wakati akizungumza na wanahabari wanawake ambao waliitembelea hifadhi hiyo ili kujifunza , kutalii na kujionea shughuli za kitalii zinavyoendeshwa katika hifadhi hiyo.

Moranda amesema licha ya hifadhi hiyo kuwa kubwa kuliko zote nchini sanjari na uwepo wa vivutio aina mbali mbali ambavyo vingeweza kuingizia serikali mapato kutoka kwa watalii wa ndani na nje lakini serikali imeshindwa kutupia jicho katika hifadhi hiyo .

Amesema hifadhi hiyo yenye ukubwa wa kilomita za mraba 45,000, hupokea watalii kutoka ndani na nje ya nchi kwa wastani wa 23,000 kwa mwaka, huku baadhi ya watalii wakilazimika kukatiza ziara yao ya kutalii katika hifadhi hiyo kutokana na kushindwa kuhimili kuifikia hifadhi hiyo kutokana na ubovu wa miundo mbinu,

Moranda amesema ili kuifikia hifadhi hiyo wageni (watalii) hulazimika kutumia usafiri wa barabara au anga, na kwamba usafiri wa barabara ungewezesha watalii wengi kutoka ndani na nje ya nchi kuifikia hifadhi hiyo kwa kuwa hata ghalama zake ni nafuu lakini kutokana na ubovu wa miundo mbinu watalii wengi wanashindwa kufika katika hifadhi hiyo kwa kuwa wengi wao hawamudu ghalama za usafiri  wa anga kutokana na ghalama zake kuwa juu ambapo mtalii analazimika kulipa dola  4000 kwa safari moja tu, na kwamba watalii wengi wa nje hutoka katika bara la Ulaya na Marekani huku wengi wao wakiwa ni watu wazima ambao wamewekeza pesa zao kwa muda mrefu tofauti na vijana ambao changamoto ya kiuchumi inaonekana kuwa ni kubwa.

Kuhusu aina za vivutio vilivyopo katika Hifadhi hiyo Moranda amesema licha ya kuwa na vivutio vingi ambavyo hupatikana katika hifadhi nyingine zilizopo nchini, Hifadhi ya Taifa Ruaha ni hifadhi ya kipekee kwani ina aina kumi (10) za simba ambao hupatikana duniani kote na ni nadra sana kuwaona katika eneo moja, kuna wanyama aina ya Tandala wakubwa na wadogo ambao unaweza kuwaona kwa wakati mmoja kitu ambacho ni adimu sana, kuna ndege aina tofauti  570, mbuni ambao hupatikana kwa wingi na kwamba kupitia mto ruaha ni rahisi kuwaona wanyama wengi kwa wakati mmoja kwa kuwa wanyama wengi hutumia mto huo kwa ajili ya kunywa maji na jambo lingine la kipekee ni utalii wa kiutamaduni pamoja na maeneo ya shughuli za kitamaduni kama matambiko.

Hata hivyo akazungumzia changamoto nyingine kubwa inayoikabili hifadhi hiyo kuwa ni kukauka kwa maji katika mto Ruaha, Moranda amesema changamoto hiyo ni kubwa na inahatarisha uhai na usalama wa wanyama kwani wanyama wengi wanakuwa hatarini kupata magonjwa kutokana na kunywa maji yaliyo tuama pia viumbe kama samaki nao wanakuwa hatarini kwani baadhi ya samaki huzimia na wengine kufa kutokana na kukosa hewa hususani pale mnyama aina ya kiboko anapojisaidia ndani ya maji kisha maji hayo yakaendelea kutuama na kuongeza kuwa changamoto nyingine ni ujangili wa kuua tembo, ujangili wa kuvua samaki, pamoja ujangili wa kuwinda ndani ya hifadhi.

Katika kukabiliana na changamoto mbali mbali kama kukauka kwa maji mto Ruaha na ujangili, hifadhi hiyo ilianzisha miradi mbalimbali kama, mradi wa kuimarisha masuala ya mazingira hususani katika maeneo ambayo yamepitiwa na bonde la ufa kama Makete, Mbarali, Wanging’ombe, Mufindi na Kilolo, mradi huo ambao kwa sasa unaingia msimu wa pili tangu kuanzishwa kwake unaojulikana kama “TUZO YA TANAPA YA KUHIFADHI MAZINGIRA” na kwamba katika maeneo yote hayo kuna kuwa na mshindi 1,2 na 3 ambao mshindi wa kwanza  hadi wa tatu hupewa kiasi cha fedha, na kufafanua kuwa sababu iliyopelekea kuanzishwa kwa mradi huo ni baada ya kugundua kuwa licha ya sababu za kisanyansi zinazopelekea maji kukauka katika mto Ruaha lakini pia shughuli za kibinadamu zinazo fanyika katika vyanzo vya maji vilivyopo katika bonge la ufa ni chanzo cha maji kukauka.

Pia Hifadhi hiyo ilianzisha mradi wa Ujirani mwema mwaka 1994, ili kudhibiti vitendo vya ujangili pamoja na kukabiliana na migogoro baina hifadhi na vijiji vinavyopakana na hifadhi hiyo na kwamba hadi sasa zaidi ya bilioni mbili (2) zimetumika ili kusaidia jamii katika sekta ya Afya, Elimu, Maji na matumizi bora ya ardhi, sanjari na miradi hiyo pia kuna miradi kama kikosi cha kufuatilia matukio kwa haraka, mradi wa mbwa wanaosaidia kufanya upekuzi wa nyara kwa haraka na muda mfupi, mradi wa kutumia wasiri,mradi wa operation tokomeza ambao umesaidia kwa kiasi kikubwa kukabiliana na vitendo vya kijangili pia hifadhi hiyo imeweka namba maalumu ambayo kila mwananchi anaruhusiwa kupiga bure muda wowote ili kutoa taarifa kwa haraka.

Moranda alimaliza kwa kuitaka serikali itupie jicho katika suala la miundo ili kuliongezea taifa pato kupitia watalii pia aliwapongeza wananchi Mkoani Iringa na maeneo jirani  kwa kuwa na uelewa kuhusu uhifadhi ambapo alimtaka kila mtanzania atambue kuwa ni jukumu lake kuzilinda mali asili zilizopo nchini kwa kuwa ndio urithi wa vizazi vya sasa na vizazi vijavyo.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni