Jumatano, 18 Mei 2016

Diwani Mkoani Katavi apandishwa kizimbani.

Diwani wa Kata ya Katumba Katika Manispaa ya Mpanda Mkoani katavi Bwn Senator Baraka Jerith (30) amefikishwa mahakamani kujibu tuhuma za Rushwa zinazomkabili.

Mapema asubuhi Tume ya kudhibiti na kupambana na Rushwa Mkoani katavi wamemfikisha diwani huyo kizimbani Kwa tuhuma za kushawishi na kupokea Rushwa jambo ambalo ni kinyume na sheria.

Mwanasheria wa Takukukuru Saimoni Buchwa aliyesaidiwa na Mwenzake Bahati Stafu Haule akisoma hati ya Mashtaka mbele ya Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya ya Mpanda Mhe Chiganga Tengwa katika kesi iliyosajiliwa kwa Na CC 1/2016

ameileza Mahakama kwamba Mshitakiwa anatuhumiwa na Makosa Mawili ambayo ni kushawishi na kosa la Pili kupokea Rushwa.

Katika Kosa la Kwanza Inadaiwa kwamba Mshitakiwa alishawishi kwa nia ya kupokea Rushwa kinyume na Kifungu Cha Sheria ya Kudhibiti na kupambana na Rushwa Kifungu cha 15(1)(a) Sheria na 11 ya Mwaka 2007 kwamba Mnamo tarehe 11/5/2016 Mshitakiwa alimshawishi ndugu CHARLES MSUKUMA kwamba atamsaidia kutohamisha mifugo yake katika eneo tengefu la makazi ya Wakimbizi la Katumba iwapo angekubali kutoa Shilingi Milioni Moja ili asitekeleze amri hiyo kama alivyoamuriwa na Mahakama ya Mwanzo Katumba yeye kama Diwani wa Kata hiyo jambo ambalo ni kinyume na Sheria za Nchi.

Katika kosa la Pili, Mshitakiwa anashitakiwa kwa Kosa la kupokea Rushwa kinyume na Kifungu cha 15(1)(b) cha Sheria ya kudhibiti na kupambana na Rushwa Na 11 Mwaka 2007.

Kwamba Mnamo tarehe 12 mwezi mei 2016 katika Mgahawa wa Mtu aitwaye Ngandieta katika Kata ya Katumba Diwani huyo alipokea kiasi cha Shilingi Laki Nne Kama sehemu ya malipo ya fedha waliokubaliana awali.

Aidha Mshitakiwa amekana Makosa yote na Mahakama kumtaka adhaminiwe Kwa masharti ya kuacha Mahakamani Pesa Taslimu Milioni mbili au Hati ya Mali isiyohamishika yenye thamani ya kulingana na fedha hiyo.

Mwanasheria wa Takukukuru Saimoni Buchwa ameiomba Mahakama kupangiwa tarehe nyingine ya kutajwa kwa Shauri hilo Kwa kuwa upelelezi wa shauri hilo haujakamilika.


Mshitakiwa amepelekwa mahabusu kwa kutotimiza masharti na kukosa wadhamini. Kesi imepangiwa tarehe 31/5/2016 itakapo tajwa tena.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni