Jumatatu, 9 Mei 2016

Kiwanda bubu cha sukari chanaswa mkoani Mbeya, hii ni baada ya mkuu wa wilaya ya Mbeya mh. Nyerembe Munasa kufanya msako mkali kufuatia agizo la Rais Magufuli la kuwafichua wafanyabiashara wanaoficha sukari!

Serikali mkoani Mbeya imekamata kiwanda bubu cha kufungasha sukari, ambacho kinadaiwa kufungasha upya sukari ya ndani kwenye mifuko yenye ujazo wa kati ya nusu kilo na kilo moja na kisha sehemu ya sukari hiyo kuuzwa nje ya nchi na nyingine kusambazwa mitaani.

Kukamatwa kwa kiwanda hicho kunatokana na hatua ya Mkuu wa Wilaya ya Mbeya, Nyerembe Munasa akiwa ameongozana na askari Polisi kuingia mwenyewe mitaani kutekeleza agizo la Rais Dk. John Magufuli la kuwasaka wafanyabiashara ambao wameficha sukari kwenye maghala.

Akiwa mitaani, ndipo akabaini uwepo wa kiwanda hicho kikiwa katika nyumba moja ya makazi ya watu iliyopo maeneo ya Soweto Jijini Mbeya, huku mifuko inayotumika kufungashia sukari hiyo ikiwa na nembo isiyoonyesha mahali sukari hiyo ilipotengenezewa.

Akizungumza baada ya kubaini uwepo wa kiwanda hicho, Munasa alisema kuwa viwanda vya aina hiyo ndivyo vinavyotumika kufungasha sukari  ambayo wakati mwingine huwa imepitwa na wakati na kuwauzia wananchi, hali ambayo inaweza kuwasababishia madhara kiafya.

“Viwanda vya aina hii ndivyo vinavyotumika kufungasha sukari feki, iliyopitwa na wakati, wao kwenye mifuko hii wanaandika tarehe nyingine ya sukari kumaliza muda wake, hali ambayo inaweza kuwadhuru watumiaji,” alisema Munasa.

Aidha Munasa alimuuliza Mmiliki wa kiwanda hicho, Bushir Sanga kama ana kibali kutoka kwenye viwanda vya ndani vinavyompa mamlaka ya kubadilisha jina la sukari, ambapo alisema kuwa hana kibali cha kutoka kwenye viwanda kinachomruhusu kufanya hivyo.

Hata hivyo Sanga ambaye pia ni mfanyabiashara maarufu wa sukari Jijini Mbeya alidai kuwa ana kibali cha kufanya shughuli hiyo kutoka Mamlaka ya Chakula na Dawa (TFDA), na pia anatambuliwa na Mamlaka ya Mapato Tanzania kwa kuwa huwa analipa kodi.

“Ninayo leseni ya TFDA na pia huwa nalipa kodi hivyo natambuliwa hata na TRA hivyo shughuli yangu ya kufungasha sukari ni halali kisheria,” alisema Sanga.

Maelezo hayo hayakutosha kumshawishi Mkuu wa wilaya kuwa mfanyabiashara huyo hana kosa, hivyo akawaamuru askari wa Jeshi la Polisi kumkamata na kumfikisha kituoni ili achukuliwe maelezo na baadaye afikishwe kwenye vyombo vya sheria ili sheria ifuate mkondo wake.


Kutokana na uhaba wa sukari uliolikumba Taifa, Rais Dk. John Magufuli ameviagiza vyombo vya dola kuwatafuta na kuwakamata wafanyabiashara ambao wameficha sukari kwenye magahala ili bidhaa hiyo ionekane ni adimu na hatimaye iweze kupanda bei.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni